Country Fm Iringa 88.5 Iringa,91.1 Mbeya
Home » » Upinzani: Kura ya maoni ni hewa.

Upinzani: Kura ya maoni ni hewa.

Kambi ya upinzani bungeni imesema hakuna uhakika Katiba inayopendekezwa itakuwa ndiyo Katiba Mpya ya Tanzania.
 
Kwa mujibu wa maoni ya msemaji mkuu wa kambi hiyo kwa Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano), Tundu Lissu, tatizo la msingi hapo ni matakwa ya Sheria ya Kura ya Maoni, 2013.
 
Alikuwa akiwasilisha maoni ya kambi hiyo bungeni kuhusu mpango na makadirio ya mapato na matumizi ya fedha ya Ofisi ya Makamu wa Rais kwa mwaka 2015/16.
 
Alisema sheria hiyo imeweka utaratibu mgumu wa uendeshaji wa kura ya maoni, ambapo kila hatua inayotakiwa kuchukuliwa haiwezekani kuahirishwa wala kuongezewa muda.
 
“Kwa mfano, ndani ya siku 14 tangu tarehe ya kupokea Katiba Inayopendekezwa, Rais anatakiwa – kwa amri iliyotangazwa katika Gazeti la Serikali na baada ya kushauriana na Rais wa Zanzibar – kuielekeza Tume ya Uchaguzi kuendesha kura ya maoni juu ya Katiba Inayopendekezwa,” alisema.
 
Alisema amri ya kura ya maoni inatakiwa kufafanua kipindi cha kampeni na kipindi ambacho kura ya maoni inatakiwa kufanyika.
 
Alisema Rais Kikwete alikwishatoa amri kwa mujibu wa kifungu cha 4 cha Sheria ya Kura ya Maoni lakini Rais hana mamlaka yoyote, kwa mujibu wa sheria hiyo ya kutengua amri yake au kutoa amri mpya ili kuwezesha kura ya maoni kufanyika kwa tarehe nyingine tofauti na tarehe iliyotangazwa kwenye amri ya  kwanza.
 
Aliongeza ndani ya siku saba baada ya kuchapishwa kwa Katiba Inayopendekezwa, Tume ya Taifa ya Uchaguzi inatakiwa kuandaa swali la kura ya maoni na kulichapisha katika Gazeti la Serikali.
 
“Na ndani ya siku 14 baada ya kuchapisha swali hilo, Tume inatakiwa kutoa taarifa ya kufanyika kwa kura ya maoni, itakayoeleza kipindi cha kuhamasisha na kuelimisha umma juu ya kura hiyo na siku ya kura ya maoni,” alisema.
 
Alisema kila msimamizi wa kura anatakiwa ndani ya siku 21 baada ya kuchapishwa kwa taarifa ya Tume, kuwajulisha wananchi katika jimbo lake la uchaguzi kuhusu utaratibu wa kufanyika kwa kura ya maoni.
 
CHANZO: NIPASHE
Ahsante kwa maoni yako,endelea kusikiliza redio country fm Iringa-One community
Facebook Blogger Plugin: Bloggerized by Joseph Kipangula Enhanced by Joseph Kipangula

0 comments:

Post a Comment

SIKILIZA COUNTRY FM

Pages

Pages

radio country fm,one community. Powered by Blogger.